Monday, February 5, 2007

USIRIDHIKE NA MTAZAMO WA JUU-JUU TU



TURIDHIKE NA MTAZAMO WA KIJUU-JUU TU?





Na William Shao

NILIPOSOMA makala katika gazeti RAI toleo la 689 yenye kichwa cha habari: PRINCESS DIANA ALIFARIKI DUNIA KWA AJALI YA MUNGU YUPI? Nilisukumwa na hitimisho la mwandishi lililosema: “Kwa vyovyote kifo cha Princess Diana ni ajali iliyotokana na Mungu.”

Mwandishi aliyesema makala hayo yaliandikwa kwa msaada wa “mashirika ya habari”, aliridhika na ripoti ya kurasa 832 ya Lord (Sir John) Stevens iliyoonyesha kuwa Princess Diana alikufa katika ajali ya kawaida “na si kwamba aliuawa na Serikali ya Uingereza ama ukoo wa kifalme.”

Sisemi ripoti ilidanganya, nasema tutazame matukio ya uhakika bila kugusa au kuridhika na ripoti hiyo. Hiyo ni ripoti ya serikali na serikali ingejitahidi isijishutumu yenyewe.

Hata hivyo, udadisi hautoshi kuishia katika ripoti tu. Habari peke yake hazitoshi kutufunua akili bila kwanza kutazama utondoti na mambo mengine madogo madogo yaliyotengeneza habari au ripoti hiyo. Ni kweli Diana alikufa katika ajali ya gari, lakini tunajuaje kuwa ajali hiyo ni “iliyotokana na Mungu” au iliyopangwa na mwanadamu?

Ikiwa wale wanaodai Princess Diana aliuawa ni ‘wenda-wazimu’, Diana mwenyewe alikuwa ‘mwenda-wazimu’ wa kwanza na kiongozi wa Libya, Muammar Gaddafi, alikuwa wa pili.

Miezi kumi kabla ya kifo chake Diana aliandika barua iliyosomeka: “Kipindi hiki cha maisha yangu ni cha hatari sana kwangu” na kudai Ufalme wa Uingereza unamwandalia kifo cha ajali ya gari. (Mirror la Uingereza Okt. 20, 2003).

Jumanne ya Septemba 2, 1997—siku mbili baada ya kifo cha Diana—Gaddafi alidai kuwa Serikali ya Uingereza na washirika wake walimuua Diana. Walimwengu tulimchukulia kiongozi huyo kama ‘mpayukaji’.

Ukitazama kwa makini mazingira yanayozunguka kifo cha Diana utaona mambo mawili: Moja ni ‘mazingira ya kisiasa’ na la pili ni ‘mazingira ya ibada za kishetani’. Kwa kuwa nafasi ni finyu, najadili hili la ‘mazingira ya kisiasa’, na hilo la pili naliacha kiporo. Katika mijadala inayokuna kama hii ndipo mtu anapoonekana mwenda-wazimu.

Princess Diana na Dodi Fayed walitumbukia rasmi katika mapenzi Jumanne ya Juni 3, 1997. Siku 38 baadaye, Ijumaa ya Julai 11, 1997, Princess Diana aliwasili kwenye nyumba ya shamba la Mzee Al Fayed yenye bustani kubwa eneo la San Tropez, kusini mwa Paris, Ufaransa, akiwa na watoto wake, William na Harry.

Wakati huo Dodi Fayed alikuwa chumbani kwake na mchumba wake, Kelly Fisher, mwanamitindo wa Mmarekani. Dodi hakuwakutanisha Kelly na Diana. Wakati Baadaye Diana akiwa katika boti, ndege binafsi ilitumwa kwa ajili ya Kelly. Diana na Kelly hawakujuana.

Kelly alikasirika sana alipogundua kuwa Dodi alimzubaisha ili apate nafasi ya kumtongoza Diana. Hatimaye Diana alirejea Uingereza na watoto wake. Ndipo siku 20 baadaye, Alhamisi ya Julai 31, Diana akarejea tena San Tropez, wakati huu akiwa bila watoto wake. Bado hakujua Dodi alikuwa na uhusiano na Kelly hadi aliposikia katika vyombo vya habari.

Siku hiyo, Julai 31, Kelly Fisher alikuwa Los Angeles, Marekani, akijiandaa kwa ajili ya harusi kati yake na Dodi Fayed iliyokuwa imepangwa kufanyika Jumamosi ya Agosti 9, 1997. Lakini siku mbili kabla ya hapo akavisikia vyombo vya habari duniani vikitangaza mapenzi kati ya Dodi na Diana. Huo ukawa mwisho wa Dodi na Kelly.

Jumba hilo la kifahari lilikuwa limefungwa vinasa sauti kufuatilia mazungumzo ya Diana. Kila alichozungumza Diana hakikuwa siri kwa wale waliomfuatilia. “Ulikuwa ni utendaji wa aina ya peke yake,” akasema Henry Porter, mhariri wa jarida Vanity Fair, akimkariri Bob Loftus aliyewahi kuwa mkuu wa usalama wa Mohamed Al Fayed.

Kwanini alikuwa akifuatiliwa kiasi hicho? Ni nani walikuwa wakimfuatilia. Ni siri gani walihitaji kutoka kwake?

Wakati Diana anaanza masaa matatu ya mwisho ya uhai wake, saa 3.47, ulizuka uvumi kwamba alikuwa na mpango wa kufunga ndoa na Dodi. Kisha uvumi huo ukawavuta hata mapaparazi (wapiga picha) kupata picha za wapenzi hao.

Dakika za mwisho za maisha yake zilianzia Hotel Ritz Paris inayomilikuwa na Al Fayed. Ulinzi aliokuwa nao—gari aina ya Range Rover iliyokuwa na watu wa kumlinda ikifuata nyuma ya gari alimokuwamo—uliondolewa. Kwa hiyo ulinzi wake ulipunguzwa.

Kwanini ulinzi ulipunguzwa ikiwa tayari ilijulikana kulikuwa na mapaparazi waliokuwa wakimwandama? Kama ilivyokuwa kwa Diana, hata wakati Rais John Kennedy alipouawa, ulinzi wake ulipunguzwa.

Gari la Kennedy halikuwa na walinzi, lakini lililokuwa nyuma yake lilikuwa na ulinzi mkali. Inasemekana hiyo ndiyo mbinu inayotumika katika mauaji ya aina hiyo. Kennedy alikuwa amepanda gari lililokuwa wazi katika mji uliokuwa hatari bila walinzi.

Wakati mtetezi wa haki za binadamu, Martin Luther King, alipouawa eneo la Memphis, Tennessee, Marekani Alhamisi ya Aprili 4, 1968, polisi mwenye asili ya Kiafrika aliyekuwa akimlinda bila kupenda alilazimishwa kuondoka kazini saa chache kabla King hajapigwa risasi.

Zimamoto wawili wenye asili ya Kiafrika waliokuwa katika kituo karibu na Lorraine Motel alimouawa Luther walihamishiwa kituo kingine cha saa chache kabla ya tukio.

Baada ya mauaji dunia ikaambiwa kuwa James Earl Ray (40) ndiye muuaji wa Luther. Lakini hata familia ya Luther haikuamini kama James Ray alihusika na kifo cha Luther. Hadi leo matokeo ya chunguzi nyingi za kifo hicho zinatatanisha.

James Ray alipofariki dunia Alhamisi ya Aprili 23, 1998, baadhi ya wanafamilia wa Martin Luther waliohudhuria mazishi yake walimlilia Ray, wengine wakisema hawana imani kwamba alihusika na kifo cha Luther.

Wakati mwanasiasa na mwanasheria wa mazingira wa Marekani Robert (Bobby) Kennedy alipouawa Jumanne ya Juni 4, 1968, mara baada ya hotuba yake katika Ambassadors Hotel mjini Los Angeles, Marekani, mpangilio wa ulinzi wake ulivurugwa—ndipo akauawa.

Mipango ilikuwa kwamba baada ya hotuba yake angetoka ukumbini kwenda nje kupita katikati ya kundi la watu, lakini alipomaliza hotuba ‘wasaidizi’ (wauaji!?) wake, hususan Frank Mankiewicz, alisisitiza kuwa ilikuwa ni salama kwake kutoka ukumbini kwa kupitia jiko la hoteli badala ya katikati ya umati wa watu.

Kennedy alipofika jikoni ndipo alipokutana na “muuaji” wake, Sirhan Bishara Sirhan, akiwa na bunduki mkononi. Hata hivyo, upelelezi binafsi unadai kuwa Robert Kennedy aliuawa na walinzi wake, hususan Thane Eugine Caesar.

Wapelelezi wengine wanasema Thane Caesar, ambaye alipaswa kumlinda Kennedy, ndiye aliyemfyatulia risasi tatu zilizohitimisha uhai wake. Upelelezi mwingine ulipoanza kugundua mambo mengine, vielelezo vingi vilifichwa.

Frank Mankiewicz, ambaye alimwongoza Robert Kennedy kwenda jikoni alikouawa, awali alikuwa msemaji wa tawi la Shirika la Kijasusi la Israel (Mossad) nchini Marekani lijulikanalo kama Anti Defamation League.

Wakati Waziri Mkuu wa Israel, Yitzhak Rabin, alipouawa Jumamosi ya Novemba 4, 1995 mjini Tel Aviv, ilidaiwa, kwa mujibu wa filamu ya tukio hilo, ulinzi wake ulisogezwa nyuma kuruhusu muuaji—au wauaji—kumpata mlengwa wao.

Hayo ndiyo yalitokea katika zile dakika, au saa, muhimu sana katika maisha ya Diana. Ama ulinzi uliondolewa au haukuondolewa, lakini hakuwa na ule ulinzi kama wa siku zote alipokuwa Paris. Ulinzi huo ulikwenda wapi? Nani aliuondoa? Kwanini?

Kwa siku nzima ya Agosti 31 alipokuwa jijini Paris, tangu Julai 31, Diana alisafiri katika gari hilo hilo, Mercedes Benz, likisindikizwa kwa nyuma na gari lingine aina ya Range Rover lililokuwa na walinzi. Walinzi hao walikwenda wapi Diana alipoikaribia mauti yake? Kwanini wasiwepo wakati wa kufa kwake?

Mercedes Benz aliyokuwa akisafiria kwa siku nzima siyo Mercedes Benz ile ile aliyopata nayo ajali. Kwanini ilibadilishwa? Jibu la swali hili linaweza kueleza mambo mengi muhimu.

Badala ya Mercedes Benz ambayo Diana alikuwa akiitumia na Dodi hadi mchana wa siku hiyo, lililetwa gari lingine (Mercedes) muda mfupi kabla mauti haijapiga hodi.

Tofauti na lile la mwanzo lililoegeshwa lango la mbele, hili la pili lilipelekwa lango la nyuma la hoteli. Gari hilo ni la kampuni ya kukodisha magari inayojulikana kama Etoile Limousines (inadaiwa inamilikiwa na Al Fayed).

Hili gari lililoletwa baadaye, Mercedes Benz S-280, lilikuwa na vioo vya giza tofauti na Mercedes Benz S-600 waliliokuwa wakitumia tangu alipowasili Paris Julai 31 ambalo halikuwa na vioo vya giza. Magari mengine yangeweza kupatikana kutoka katika kampuni hiyo, lakini hili lilifaa zaidi. Kwanini?

Akihojiwa na wapelelezi wa kifo cha Diana, Mkurugenzi wa Etoile, Niels Siegel, alisema yeye ndiye aliyelipeleka gari hilo lango la nyuma la hoteli ya Ritz badala ya lango la mbele, lakini wapelelezi wengine waligundua kuwa alikuwa akidanganya. Kisha wakaanza kuwa na wasiwasi.

Iligundulika kuwa aliyelipeleka gari hilo siyo Siegel, bali ni dereva aliyeitwa Frederic Lucard. Ilijulikana hivyo baada ya kuonekana katika kamera za hoteli hiyo siku ya tukio. Kama hakukuwa na jambo la kuficha, kwanini mkurugenzi wa Etoile alidanganya?

Lucard alipobanwa na mmoja wa wapelelezi alionyesha kushangazwa sana kwa kampuni “makini” kama Etoile kumruhusu mtu kama Henri Paul (dereva aliyewaendesha Diana na Dodi hadi vifo vyao) kuendesha magari ya kampuni hiyo kwa sababu “hakuwa amefuzu kama dereva...”

Gari hilo likiendeshwa na Henri Paul, likiwa na Diana na Dodi (wakiwa kiti cha nyuma) pamoja na mlinzi wao, Trevor Rees-Jones, liliondoka lango la nyuma la Ritz saa 6:20 usiku.

Kufika katika taa za barabara ya Place de la Concorde, inasemekana kuwa paparazzi mmoja, Romuald Rat, akiwa katika pikipiki, aliiona gari ikisimama kidogo na kisha kupita kwa kasi kwenye taa nyekundu kuelekea barabara ya Cours la Reine kandokando ya Mto Seine. (rejea kiungo hiki cha tovuti: http://www.wethepeople.la/diana13.htm )

Baadaye kidogo gari ilipoteza mwelekeo kisha ikagonga nguzo ya 13 ya barabara ya chini kwa chini ya Ponte de L’Alma. Henri Paul na Dodi Fayed walifariki dunia papo hapo. Diana alifariki dakika kadhaa baadaye.

Ingawa wengi wanaamini kwamba ‘wapenzi’ hawa walikuwa wakielekea katika nyumba ya Dodi iliyoko karibu na Arc de Triomphe wakitokea Hotel Ritz, ukitazama ramani ya Paris (Paris Guide Map) ukweli ni kwamba hawakuwa wakielekea kwa Dodi bali walikuwa wakienda upande ulio kinyume na huo.

Mara baada ya ajali hiyo, mambo mengi yalitendeka hadi Diana alipotangazwa rasmi kwamba amefariki dunia. Upelelezi fulani fulani unaonyesha kuwa alikuwa akiongea hata dakika kadhaa baada ya ajali, lakini haijaelezwa alichozungumza.

Ingawa Diana na Dodi walipata ajali katika gari moja, mwili wa Diana ulifanyiwa uchunguzi lakini ule wa Dodi haukufanyiwa. Hii inatuleta kwenye swali lingine. Kwanini Dodi hakufanyiwa uchunguzi kama Diana ikiwa wote wawili walihusika katika ajali ile ile moja? Uchunguzi aliofanyiwa Diana lakini asifanyiwe Dodi ulikuwa wa nini?

Kuna wanaodai kuwa Diana alikuwa na mimba ya Dodi. Huenda hili si la kweli kwa sababu ni Diana peke yake, na pengine Dodi, angeweza kukiri au kukanusha. Lakini namna gani ikiwa watatokea “wenda-wazimu” wengine wakasema kuwa uchunguzi aliofanyiwa Diana ni kuhakikisha kuwa mimba aliyokuwa nayo inaondolewa ili kupoteza ushahidi wa kwamba alikuwa nayo? Hawa tutawaita “wehu”?

Ni vigumu kujua kama Diana alikuwa na mimba. Lakini Ijumaa ya Septemba 19, 1997, jarida TIME lililikariri shirika la habari la Ufaransa Agence France-Presse (AFP) likisema kwamba hadi siku ya ajali “huenda Diana alikuwa na mimba ya wiki sita.” Gazeti The Chicago Tribune (Julai 15, 1997) lilimripoti Diana akiwaambia waandishi hivi:

“Mtapata mshangao. Mtaona. Mtashangaa mtakapoona jambo nitakalofanya.” Alikuwa akizungumza kuhusu ujauzito wake? Alikuwa akigusia kuoana na Dodi? Jibu lolote kwa maswali hayo ni la kubuni.

Jarida TIME (Sept. 8, 1997) lilimkariri Frederic Maillez, tabibu wa dharura aliyekuwa wa kwanza kufika eneo la ajali, akisema kuwa wakati fulani (wakati hajakata roho) Diana alitamka kuwa alikuwa na mimba ya wiki tatu huku akishika tumbo lake. Inawezekana kuna mambo mengi alisema, lakini hatutaambiwa aliyosema.

Mmoja wa watu waliofanya upelelezi juu ya ajali hiyo ni polisi mstaafu aliyeitwa John Stalker. Aliposokia watu wakisema Serikali ya Ufaransa imekula njama ya kumuua Princess Diana, aliingiwa na swali moja la msingi:

“Kwanini Serikali ya Ufaransa imuue mwanamke wa Uingereza?” Stalker alianza kwa kuukataa uwezekano wa njama. Lakini kadiri muda ulivyopita aliingiwa na mashaka zaidi.

“Kwanini usalama wote wa Fayed aliopewa Diana ulipunguzwa hadi kufikia mlinzi mmoja asiyeaminika (Rees-Jones) na bila gari ya kusindikiza? Kwanini polisi haikuomba msaada kutoka kwa umma? Kwanini mwili wa Dodi Fayed haukufanyiwa uchunguzi?” Nilisoma maswali aliyokuwa akiuliza, lakini sijui kama aliwahi kupata majibu.

Baada ya ajali hiyo, wataalamu wa magari ya Mercedes Benz waliiomba serikali ya Ufaransa walifanyie uchunguzi gari hilo, lakini maofisa wa serikali walikataa. Kwanini? Lilikuwa na kasoro gani? Kitu gani kilikuwa kinafichwa hapo? Kama walitaka mambo yawe wazi kwanini walikataa ombi hilo?

Kama ilivyo katika mambo mengine yanayofanana na hili, kisingizio, au ‘kisababishi’, kilipatikana. Jambo la kwanza kufanyika ni kutuhumu watu.

Ikasemwa kuwa dereva Pauli Henri ni chanzo kwa sababu alikuwa amelewa kupita kiwango kinachoruhusiwa kisheria nchini Ufaransa. Lakini uchunguzi ukaonyesha hakuwa amevuka kiwango cha ulevi. Baadaye kidogo wimbo ukabadilika. Paparazzi ndio chanzo.

Kuna zaidi ya hayo. Inasemekana kuwa katika Jiji la Paris, moja ya miji sita mikubwa zaidi duniani, kuna kamera nyingi zilizoko maeneo yote ya barabara jijini humo—hasa eneo la Ponte de L’Alma ilipotokea ajali.

Ikiwa kamera hizo zingekuwa zinafanya kazi usiku huo ingekuwa ni rahisi kumaliza ubishi wote kwa sababu picha zake zingeonyesha kilichotokea na namna kilivyotokea.

Kamera moja inayotazama chini katika lango la kuingia katika barabara hiyo ya ardhini ingeweza kuona gari aina ya FIAT UNO inayodaiwa kusababisha ajali (kisingizio cha tatu), au watu waliokuwa katika pikipiki zinazodaiwa zilimfanya Henri Paul ashindwe kudhibiti gari lake.

“Lakini kamera hiyo, kama zilivyokuwa nyingine zote, ilikuwa imezimwa katika wakati huo muhimu sana,” kinasema kitabu Who Killed Diana kilichoandikwa na Simon Regan ambaye amekuwa mwandishi wa habari za uchunguzi kwa miaka 35.

Kitabu The Biggest Secret © 1999 kinasema: “Hakuna wakati mwingine wowote katika historia ya Paris ambao mfumo huu wa kamera umekuwa na hitilafu kwa wakati mmoja na polisi wakakataa kueleza kilichotokea.”

Mfumo huo wa kamera hutumia umeme unaojitegemea na unaendeshwa na polisi na, “hasa hasa,” kinasema The Biggest Secret, “mawakala wa Shirika la Kijasusi la Ufaransa, kwa sababu kamera hizo zimewekwa maeneo hayo kwa ajili ya mambo mengi zaidi ya kutazama magari tu.”

Wakati huo huo ambao mfumo huo wa kamera ulipofeli, mawasiliano yote ya redio za polisi katika maeneo ya kati ya Paris yalizimika. Kwanini mambo hayo yatokee kwa wakati mmoja, hasa katika dakika chache kuelekea kifo cha mwanamke maarufu zaidi duniani?

Swali linaweza kuzuka. Kama Diana aliuawa, nani aliyeandaa mauaji hayo? Anayetoa amri ya kuua si lazima awe muuaji. Katika mtandao—au tuseme utando, buibui anaweza kuandaa mipango, lakini mipango hiyo ikatekelezwa na nzi, pengine bila nzi huyo kutambua.

Wanaoandaa kile kinachoitwa ‘nadharia ya kigwena’ wana mambo mengi zaidi ya kuzungumza, na ni mambo ambayo dunia inahitaji kujua.

Kwa mfano, kuna ushahidi kwamba Rais John Kennedy hakuuawa na Lee Harvey Oswald kama ilivyodaiwa awali, bali aliuawa na mtu kutoka Kikosi cha Jeshi la Siri (OAS) la Ujasusi la Ufaransa na, ushahidi mwingine unadai, wauaji hao walipata mafunzo kutoka kwa “muuaji mkuu” wa Mossad (Israel) katika Bara la Ulaya aliyeitwa Yitzhak Shamir.

Kwa mujibu wa Encyclopedia of Terrorism © 2002, miaka 20 baada ya mauaji ya Kennedy Novemba 1963, Shamir akawa Waziri Mkuu wa Israel (1983-1984 na 1986-1992) hadi aliposhindwa na Yitzhak Rabin katika uchaguzi wa 1992. Alikuwa mpinzani wa Rabin, je, alishiriki katika kumuua? Ni vigumu kujua!

Sven Olof Joachim Palme, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Sweden, inadaiwa—hii haijathibitishwa—wauaji wake walipokea amri ya mauaji kutoka kwa Baba George Bush. Mauaji hayo yalitekelezwa na majasusi wa Afrika Kusini wanaojulikana kama BOSS (South African Bureau Of State Security).

Wizara ya Mambo ya Nje ya Uingereza ina kikosi chake cha siri (cha mauaji) kinachojulikana kama Group 13. Ujasusi wa Uingereza una vikosi kama MI5 (Military Intelligence 5) ambacho kinashughulikia ‘usalama’ wa ndani na MI6 (Military Intelligence 6) kinachoshughulikia mambo ya nje.

Mwaka 1998 MI5 kilidai kuwa hakiui watu. Lakini haiwezekani inatuma wengine waue badala yake? Kauli hiyo ilikuja baada ya ofisa wa MI5, David Shayler, kufichua siri kwamba MI6 ilikula njama za kumuua Kanali Gaddafi wa Libya.

Jaribio hilo lilishindwa kwa sababu bomu lililokusudiwa lilitegwa kwenye gari tofauti na alilopanda Gaddafi. Hii ilikuwa Februari 1996. Gaddafi alinusurika, lakini watu kadhaa waliuawa.
Miaka kumi kabla ya hapo, Jumanne ya Aprili 15, 1986, Gaddafi alinusurika wakati ndege za Marekani, zikitokea Uingereza, zilipokusudia kumuua yeye na familia yake. Ingawa hakuuawa, raia 55 wasio na hatia mjini Tripoli, pamoja na binti mmoja wa Gaddafi, waliuawa katika shambulio hilo.

Shayler aliiambia BBC kwamba MI6 ilipenyeza dola 160,000 za Marekani kwa Waislamu wenye msimamo mkali wamuue Gaddafi. Shayler alipotaka kuzungumza katika TV kuhusu ukweli wa ‘ajali’ ya Princess Diana, aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Robin Cook, alimzuia. Baadaye Shayler alikamatwa mjini Paris na kupelekwa London, Uingereza.

Chanzo kingine kinadai kuwa MI6 ilipanga kumuua aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Yugoslavia, Slobodan Milosevic, mwaka 1992 kwa ajali ya gari. Waliposhindwa, walitumia mabomu ya NATO mwaka 1999. Kama ni kweli walipanga mauaji ya wakuu wa nchi, sembuse Diana?

Chanzo muhimu cha Serikali ya Ufaransa kililiambia jarida The People (Nov. 9 1997) kwamba kulikuwa na “…angalau maofisa (majasusi) sita wa MI6 katika Ubalozi wa Uingereza mjini Paris mwisho wa juma lile la kifo cha Diana …angalau ofisa mmoja kati ya hao alionekana akiwafuatilia Diana na Dodi baada ya kuwasili kutoka katika mapumziko huko Sardinia.”

Gazeti Daily Mail (Des. 4, 2004) la Uingereza lilifichua kuwa dereva Henri Paul, ambaye naye alifariki katika ajali, alikuwa akilipwa na MI6. Upo hapo? Hii ilijulikana wakati wa upelelezi wa kamishina wa Scotland Yard, Sir John Stevens. Lakini Stevens alikumbana na vikwazo kwa sababu kuhoji maofisa wa MI6 kulihitaji kwanza ridhaa ya mkuu wa MI6, John Scarlett.

Mwaka 2003, Paul Burrell, aliyekuwa mtumishi wa Princess Diana na rafiki yake mkubwa, alisema miezi kumi kabla ya ‘ajali’ hiyo alipata barua kutoka kwa Diana ikisema kuwa kulikuwa na njama za kumuua kwa ajali ya gari.

“Kipindi hiki cha maisha yangu ni cha hatari sana kwangu,” barua hiyo ilisema na kudai kuwa hatari kubwa ni kwamba “Prince Charles anaandaa ‘ajali’ katika gari langu, …”

Kama MI6 walimuua Diana, basi walitumwa, na kama ndivyo, waliwashirikisha wenzao wa Ufaransa. Lakini ikiwa walikula njama ya kumuua Diana, wangepata faida gani kutokana na kifo chake? Yako mengi, lakini tazama haya mawili tu.

Kwanza, Princess Diana alikuwa tayari ameanza kuwa mtu hatari kwa familia ya Ufalme wa Uingereza kwa sababu alijua siri nyingi sana za familia hiyo na alikuwa ameshaanza kuzianika.

Pili, “Serikali ya Uingereza haikuweza kuvumilia wazo la kwamba Diana—akiwa katika mapenzi na Mwislamu wa Misri—angeweza kubadili dini na kuwa Mwislamu, kwa hiyo ilibidi aondoke…” (Independent on Sunday, Okt. 12, 1997).

Pengine haya si mambo muhimu ya kuandika, lakini tunajua kuwa yanatuathiri sote. Pengine tungezingatia hoja na mambo mengi kuhusu kifo cha Diana, hitimisho letu lisingekuwa hivi: “Kwa vyovyote kifo cha Princess Diana ni ajali iliyotokana na Mungu.”

No comments: